Connect with us

Klabu ya soka kutoka nchini Uingereza Everton FC, imewasili jijini Dar es salaam nchini Tanzania, tayari kumenyana na Gor Mahia ya Kenya katika mchuano wa kimataifa wa kirafiki siku ya Alhamisi katika uwanja wa Taifa.

 Mchuano huu umeandaliwa na kampuni ya michezo ya kubahatisha kutoka nchini Kenya ya Sportpesa, inayofadhili timu hizo mbili.

Gor Mahia mabingwa ligi ya Kenya mara 15 waliwasili jijini Dar es salaam siku ya Jumanne.

Wanacheza na klabu ya Everton baada ya kushinda makala ya kwanza ya taji la Sportpesa lililoshirikisha vlabu kutoka Tanzania na Kenya mwezi Juni.

Mchuano huo wa kirafiki wa Gor Mahia, utakuwa wa kwanza kwa kocha mpya Dylan Kerr.

Everton iliyomaliza nafasi ya saba katika michuano ya ligi kuu nchini Uingereza msimu uliopita, inatumia mchuano huu kama maandalizi ya msimu mpya mwezi Agosti.

Mchuano huu unakuja wakati huu mshambuliaji wa zamani wa Mancheter United Wayne Rooney, akihamia katika klabu hiyo aliyoichezea akiwa na miaka 13.

More in